Header Ads

Mbeya City kutembeza bakuli ni aibu


Mbeya. Mbeya City ni miongoni mwa klabu zinazozungukwa na neema ya kuwa na udhamini mnono hata kuzipiku timu Kongwe za Simba na Yanga lakini cha kushangaza timu hiyo kwa sasa choka mbaya.

Achana na udhamini wa Vodacom na Azam zilizonazo timu zote 16 zilizoshiriki ligi kuu kwa msimu huu lakini wao (Mbeya City) wana dhaminiwa na Binslum, Sports Master, Cocacola pamoja na  Bhojan Chemistry anayetoa dawa kwa wachezaji pindi wanapoumia.

Lakini cha kushangaza kwa msimu huu timu hiyo imefikia hatua mbaya kiuchumi,hali iliyowafanya madiwani wa  Halmashauri ya Jiji la Mbeya ambao ndiyo wamiliki wa timu hiyo kuingilia kati ili kunusuru hali hiyo.

Hali ya ukata  kwa siku za hivi karibuni imesababisha kwa baadhi ya wachezaji kutolipwa mishahara yao ya miezi miwili hadi mitatu na hii inawezekana ndiyo chanzo haswa cha timu kuvurunda msimu huu.

Kutokana na hilo madiwani waliamua kuweka mambo wazi kuhusu timu kukabiliwa na ukata na kutakiwa kuichangia klabu yao kwani bila mabosi hao mambo hayawezi kwenda sawa. 

Katika kikao cha Baraza la madiwani  wa halmashauri ya jiji kilichofanyika hivi karibuni ,  Mwenyekiti wa kamati ya huduma za jamii wa Mbeya City,Fanuel Kianula   alitangaza mbele ya baraza hilo kuwa kila diwani anatakiwa kuichangia Klabu  kiasi cha Sh20,000 .

Lengo kubwa  la madiwani hao kutakiwa kuchanga fedha ni kwa ajili ya kuisaidia klabu kumaliza msimu vizuri na kumalizana na wachezaji wao.

Hali ya ukata ilianza kwa mabingwa watetezi wa ligi hiyo (Yanga) huku jinamizi hilo likihamia kwa Mbeya City ambayo katika akili za wadau na wapenzi wa soka haiwezi kupenya kwamba klabu hiyo  inatembeza bakuli.

Na hii inaniaminisha kuwa kipindi cha duru la pili la msimu huu  timu inapovurunda na kupata sare zaidi ya nne mfululizo kuna baadhi ya wachezaji walidokeza kuwa wanadai mishahara yao lakini pia posho zenyewe ilikuwa shida kuzipata kumbe ukata ulikuwepo ila viongozi wake walivunga tu kuweka mambo wazi.

Kwa mujibu wa Katibu wa klabu hiyo Emmanuel Kimbe, inadaiwa kuwa bajeti ya kuendesha timu inagharimu Sh1.2 bilioni  kwa msimu mmoja ,hii ikiwa ni mishahara,posho pamoja  na chakula kwa wachezaji wakiwa kambini.

Najiuliza Mbeya City  hii hii yenye wadhamini  hata kuzipiku klabu kongwe hapa nchini za Simba na Yanga imekuwaje leo hii itembeze bakuli kwa watendaji wake wa halmashuri hata kama ndiyo wamiliki? 

Mapema Aprili mwaka huu imeongeza mdhamini wanne ambaye ni Sports Master atakayetengeneza na kuuza jezi zao kwa misimu miwili yaani kuanzia msimu ujao wa ligi .

Mamilioni yanayotolewa na wadhamini hao yanafanya kazi gani hadi madiwani wake waanze kuichangia timu hiyo inayotamaniwa na vilabu vingi vinavyopiga miayo ya njaa hapa nchini.

Kwa fikra zangu nilijua huu ni wakati wa klabu hiyo kupumua kuhusu mambo ya kifedha na sasa ielekeze nguvu na akili jinsi ya kumaliza mechi hizo mbili zilizoshika majibu ya wao kusalia ama kwenda na maji.

Lakini tunapata taarifa ya kwamba ukata uliopo ni balaa labda  Mungu tu asimame ili wachezaji wamalize msimu huu vyema na kila mmoja aondoke akiwa hana dukuduku na mtu .
Haiwezekani kwa timu pendwa kama Mbeya City kutudanganya leo hii kwamba haina fedha wakati misimu yote mitatu  tangu ianze kushiriki ligi imeendeshwa vizuri kwa nini msimu huu ilie njaa na huku imeongeza mdhamini mapema.

Na ndiyo maana matokeo ya klabu hiyo kwa misimu miwili mfululizo siyo ya kuridhisha kwani imekuwa ikipita kwenye  tundu la sindano wakati kwa msimu wake wa kwanza ilizichchafya Simba , na Yanga kupata matokeo zilipokuna  nayo.

Ni wakati wa benchi zima la ufundi wa klabu hiyo kukaa chini na kujitafakari mara mbili mbili kwamba ukata huo unatokana na nini?,

Yawezekana kuna wajanja wachache wanaotumia mwanya huo kujinufaisha wao na kusahau maslahi ya klabu inayouletea mkoa wa Mbeya heshima ya kipekee pamoja na kuzalisha ajira kwa vijana.
Ni wakati wa kuamka na kufuta makosa yote yaliyojitokeza kwa msimu huu ili yasijirudie msimu ujao kwani kulewa sifa kutatugeuzia kibao na kuwa kama timu ile iliyopanda kwa mbwembwe na kushuka kwa mbwembwe hadi leo iko wapi ?
Viongozi pamoja na benchi la ufundi hapo kuna kitu cha kujifunza na kuchukua hatua ikiwemo hii ya kutorudia makopsa yaliyompata jirani yako Tukuyu Stars amabye hadi sasa amepotea kwenye ramani ya soka.

Siku zote kuna usemi usema ‘chuki na ubinafsi ni adui wa maendeleo ’ hivyo vyombo vya dola vinatakiwa viingilie kati kufanya uchunguzi juu ya suala hili


No comments